Kwa mujibu wa taarifa, Mahakama ya Juu ya Kiislamu katika jimbo la Kano imesema kuwa Yahaya Sharif-Aminu, mwenye umri wa miaka 22, alipatikana na hatia ya kukufuru kwa wimbo wake aliousambaza kupitia mtandao wa kijamii wa WhatsApp mwezi Machi.
Jaji Khadi Aliyu Muhammad Kani alisema kuwa, Sharif-Aminu ambaye hakukanusha mashitaka, anaweza kukata rufaa.
Baada ya muziki huo kuenea katika mitandao ya kijamii, ghasia ziliibuka huku waandamanaji waliokuwa na hasira wakiteketeza moto nyumba ya famillia yake.
Inasemekana kuwa muimbaji huyo alimsifu mmoja kati ya viongozi wa Tariqa ya Tijanniya kiasi cha kumpa hadhi ya juu zaidi ya Mtume Muhammad SAW.
Majimbo ya kaskazini mwa Nigeria, ambayo aghalabu ya wakaazi wake ni Waislamu, huwa na mifumo miwili ya mahakama mmoja ni mfumo wa kawaida wa kisekula na wa pili ni ule unaotegemea sheria za Kiislamu na wanaofikishwa hapo huwa ni Waislamu tu.