Ayatullah Ali Khamenei ameyasema leo Jumamosi mjini Tehran katika shughuli ya maombolezo ya wanafunzi wa vyuo vikuu nchini Iran kwa mnasaba wa Arbaeen ya Imam Hussein na kuongeza kwamba: "Tukio la kimuujiza la matembezi ya Arbaeen haliwezi kutekelezwa kwa sera na tadibiri yoyote ya kibinadamu; na kwa tukio hili, mkono wa Mwenyezi Mungu unaotoa ishara njema kwamba njia iliyo mbele yetu iko wazi na inaweza kupitika."
Ayatullah Khamenei amesema, nyoyo safi na zenye imani za vijana ndio sababu ya kuongeza ubora wa dua na mawaidha na kuongezeka hidaya ya Mwenyezi Mungu na akasema: Shuguli ya Arbaeen ya Imam Hussein AS ambayo ni bendera ya juu ya Bwana wa Mashahidi, mwaka huu imefanyika kwa ufanisi zaidi na imekuwa kubwa zaidi kuliko kipindi kingine chochote katika historia.
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amewausia vijana kuthamini ujana wao na kuvipa kipaumbele maalumu vikao na makundi yanayojihusisha na shughuli ya kukumbuka ya mauaji ya Imam Hussein AS na akasema: Makundi hayo pia yanapaswa kubakisha hai kumbukumbu ya Ahlul-Bayt na kuwa kitovu na msingi wa kueleza haki na kweli.
Ayatullah Khamenei ameashiria njama zinazoendelea kufanywa na watu wenye nia mbaya na maharamia wanaopindisha haki na kweli kuhusu matukio muhimu kama vile maandamano yenye hamasa kubwa ya Arubaini ya Imam Hussein AS, na amewakumbusha watu wote kutekeleza wajibu wao katika uwanja huo. Amesema: Sentensi mbili muhimu na za milele za Qur'ani, yaani, himizo la kuusiana haki na lile linalohimiza kuwa na subira daima hasa katika kipindi cha sasa, ni mwongozo wa msingi.
3480516