IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Adui anapanga kujipenyeza Iran hususan kiutamaduni

6:09 - September 17, 2015
Habari ID: 3364408
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullahil Udhma Ali Khamenei amesema kuwa maadui wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wanafanya mikakati ya kubadili itikadi za jamii na kupenya katika vituo vya kutayarisha na kuchukua maamuzi hapa nchini.

Ayatullah Ali Khamenei ameyasema haya Jumatano mjini Tehran katika hadhara ya maelfu ya makamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC), maarufu kama Sepah,na kuongeza kuwa, kwa matarajio yasiyo na msingi ya kumalizika Mapinduzi ya Kiislamu, adui anafanya mikakati kupenya hapa nchini hususan katika masuala ya kisiasa na kiutamaduni, lakini kutambua vyema njama za adui, kuimarishwa moyo wa kimapinduzi na harakati ya kudumu kuelekea upande wa kutimiza thamani na matukufu vitamzuia kutimiza malengo yake.
Amesema kuwa Iran kamwe haijawa wala haitakuwa ya kwanza kuanza vita na kuongeza kuwa: Pamoja na hayo kwa kuwa Mapinduzi ya Kiislamu siku zote yanakabiliwa na hatari ya wapinzani na wakorofi, kuna udharura kwa jeshi la IRGC kuwa macho na makini daima kwa ajili ya kukabiliana na vitisho hivyo.
Ayatullahil Udhma Ali Khamenei amesema kuwa, kumtambua adui ni miongoni mwa vipengee vya kulinda Mapinduzi. Ameongeza kuwa, maana ya adui ni ubeberu wa kimataifa ambao dhihirisho na kielelezo chake kamili ni Marekani, na vibaraka wake ni tawala zilizobakia nyuma na watu dhaifu kinafsi.
Kiongozi Muadhamu amesema kuwa, maadui wa Mapinduzi ya Kiislamu ni wale ambao miaka mingi iliyopita walikuja Mashariki ya Kati kwa nara na kaulimbiu za 'kuimarisha amani', 'kupambana na ugaidi', 'kuleta demokrasia' na 'kuleta amani' lakini hii leo matunda ya kuwepo kwao hapa ni ukosefu wa amani, kujitokeza ugaidi na ukatili na kuzusha vita katika eneo hili.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekosoa vikali fikra za kipotofu na kijinga za matakfiri wanaokufurisha Waislamu na kusema: Uislamu unaotegemea akili na mapokezi, unaoegamia kwenye Qur'ani na mafundisho ya Mtume SAW na Ahlu Bait zake AS ndiyo msingi wa mapinduzi yetu na unaweza kutetewa kwa nguvu ya mantiki na kulinganiwa katika duru zote za dunia ya sasa.
Ayatullah Khamenei ametilia mkazo udharura wa jeshi la IRGC kutilia maanani vitisho vyote zikiwemo njama za adui za kutaka kupenya nchini Iran kisiasa na kiutamaduni.

captcha