Jamiat Ulama-e-Hind yenye makazi mjini Deoband jimboni Uttar Pradesh imeonyesha kusikitishwa na kuenea chuki katika jamii na kusema kuwa serikali inawafumbia macho watu wanaoeneza chuki dhidi ya Waislamu ambao ni jamii ya wachache nchini humo.
Jamiat Ulama-e-Hind imesema umoja wa nchi hiyo unatatizwa kwa jina la "utaifa bandia", ambao ni hatari sio tu kwa Waislamu bali nchi nzima.
Aidha Jamiat Ulama-e-Hind, katika kikao cha kamati yake ya usimamizi, ilipitisha azimio la kulitaka hatua zichukuliwe ''kusitisha mara moja jumbe ambazo sio tu ni dhidi ya Waislamu na Uislamu bali watu wote wanaoamini demokrasia, haki na usawa''.
Tangu serikali ya chama cha Kihindu cha Bharatiya Janata (BJP) mwaka 2014, kumefanyika mabadiliko ya akthari ya sheria kwa ajili ya kuwaridhisha Wahindu wenye misimamo ya kufurutu ada, mabadiliko ambayo yanakinzana na katiba ya India. Aidha katika kipindi cha utawala wa chama hiki kuna kesi nyingi ambazo hukumu zake zimetolewa kwa matashi ya kisiasa na kukanyaka haki za jamii za walio wachache hususan Waislamu.
Sera za serikali ya BJP za kuwakandamiza Waislamu zimewapa ubavu zaidi Wahindu wenye misimamo mikali kueneza chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu nchini humo.
Hii ni katika hali ambayo, Waislamu nchini India ndio jamii ya pili kwa ukubwa nchini humo baada ya Wahindu. Kwa muktadha huo, kuipuuza jamii ya Waislamu wapatao milioni 215 nchini India sio tu kwamba, kunaonyesha kupungua kwa uvumilivu wa kidini katika nchi hiyo tangu chama tawala cha BJP kishike hatamu za uongozi nchini India 2014, bali chama hicho kimechora rasmi mstari wa wazi wa ubaguzi dhidi ya Waislamu.
3479081