Wizara hiyo inasambaza vijitabu maalumu kwa mahujaji kuhusu ugonjwa wa Ebola ili kuzuia kuenea ugonjwa huo katika wakati huu ambao mahujaji wameanza kuingia Saudi Arabia. Msemaji wa Wizara ya Afya ya Saudia Khalid Al-Mirghalani amenukuliwa akisema kuwa wizara yake pia imetuma vijitabu hivyo kote duniani ili mahujaji wa mwaka huu waweze kuvisoma kabla ya kuelekea Saudia. Vijitabu hivyo vinatoa maelezo ambayo yanapaswa kufuatwa na mahujaji wakati wakiwa katika miji mitakatifu ya Makkah na Madinah. Saudi Arabia tayari imetangaza kuwazuia mahujaji kutoka nchi zilizoathiriwa zaidi na Ebola ambazo ni Sierra Leone, Liberia na Guinea. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), zaidi ya watu 2,300 wamekwishapoteza maisha kutokana na ugonjwa huo, huko magharibi mwa Afrika.