Kwa mujibu wa gazeti la al Diyar la Lebanon, safari ya mwanamfalme huyo kwenye eneo la Mina, ilisababisha kubadilika njia iliyoainishwa ya ya mahujaji kutoka eneo moja kwenda jingine na jambo hilo likaibua msongamano na hatimaye maafa makubwa. Al Diyaar limesisitiza kuwa, hakuna jambo jingine lililosababisha maafa hayo ya kusikitisha ghairi ya Mohammad Bin Salman Aal Saud ambaye ni mrithi wa kiti cha ufalme na Waziri wa Vita wa Saudia. "Ukweli ni kwamba, msongamano ulishadidi wakati mwanamfalme huyo alipowasili eneo la Mina kwa lengo la kushiriki ibada hiyo kwani aliandamana na walinzi 350 wakiwemo maafisa wa kijeshi 200 na askari polisi 150. Alipowasili kuliibuka msongamano mkubwa hasa kutokana kwamba njia kuu aliyoitumia ilifungwa bila ya taarifa ili kumruhusu apite. Ni hapo ndipo mwelekeo wa mahujaji ukabadilika na kukatokea mkanyagano wa kutisha." Limeandika gazeti hilo. Aidha gazeti hilo limefafanua kuwa, baada ya mwanamfalme huyo kuona maafa hayo aliondoka eneo la tukio haraka huku akiacha watu wakiendelea kukanyagana. Katika kujaribu kukwepa lawama, serikali ya Saudia, imekadhibisha habari hiyo na hivyo kuwafanya watu kushindwa kujua sababu iliyopelekea barabara kuu ya kuelekea Mina kufungwa ikiwa si safari ya mwanamfalme huyo. Katika hali ambayo Mfalme Salman bin Abdulaziz Aal Saud anasema kuwa hakukuwepo uzembe wowote katika eneo hilo, kwa upande wake mwanamfalme huyo, Mohammad Bin Salman ametaka orodha ya wasimamizi waliokuwepo eneo la Mina akisisitiza kuwa wao ndio sababu ya maafa hayo.../mh